Banne

Translate

Saturday, 30 April 2016

MAGONJWA YA KUKU .UMUHIMU WA KUZUIA NA KINGA ZA MAGONJWA

UMUHIMU WA KUZUIA NA KINGA ZA MAGONJWA



Ø  Hupunguza athari za kiuchumi zitokanazo na maambukizi.
Ø  Hulinda afya za kuku ambao hawajaambukizwa.
Ø  Hupunguza kuenea kwa maambukizi kutoka kuku wagonjwa kwenda kuku wasio wagonjwa.
Ø  Huwakinga wanadamu wasipate maambukizi kutoka kwa kuku wagonjwa.
Ø  Huzalisha kuku na bidhaa zenye ubora wa juu ambazo hupata bei nzuri sokoni.
UTEKELEZAJI WA TARATIBU ZA KUZUIA KUENEA KWA MAGONJWA
      Taratibu za Kuzuia Kuenea kwa Magonjwa hutekelezwa kwa lengo la kuzuia uingiaji na usambaaji wa vimelea vya ugonjwa ndani na kati ya vijiji, kaya na mashamba. Taratibu hizi ni pamoja na kuweka karantini ambapo magonjwa na vimelea vya ugonjwa huzuiwa kuingia katika eneo fulani, au vimelea huharibiwa na kuzuiwa sehemu moja ili
visipenye kuingia maeneo mengine. Hivyo basi, taratibu za kuzuia kuenea kwa magonjwa zina vipengele vikuu vitatu: karantini, kudhibiti njia za usafirishaji na usafi wa maeneo.
Programu imara ya kuzuia kuenea magonjwa ni muhimu sana ili uweze kuendelea kuwa na kuku wenye afya. Unapotayarisha programu hii katika shamba la kuku, vipengele vitatu vya kuzingatia ni:
1. Eneo lilipo shamba au banda: Shamba au banda la kuku liwe mbali na mashamba mengine ya ndege na mifugo mingine. Ni vyema banda moja likawa na kuku wa umri mmoja ili kuzuia vimelea vya magonjwa
kuendelea kubaki bandani.
2. Ramani ya shamba au banda: Kujenga uzio ili kuzuia watu wasiohusika kuingia shambani au bandani. Mchoro wa mabanda upunguze pita pita za watu na uwezeshe usafi na upuliziaji wa dawa kufanyika kwa urahisi. Jenga mabanda yenye nyavu ambayo ndege pori na panya hawawezi kuingia.
3. Taratibu za kuendesha shughuli za shamba: Zuia kuingizwa na kuenezwa kwa magonjwa shambani
kwa kudhibiti uingiaji wa watu, vyakula, vifaa, wanyama na magari ndani ya shamba.

Hatua za Tahadhari za Kuzuia Kuingia na Kuenea kwa Magonjwa Shambani
Ø  Tenganisha ndege kufuatana na aina ya ndege na umri wao
Ø  Weka karantini kwa ndege/kuku wapya ili wachunguzwe kwa kipindi kisichopungua wiki mbili
kabla ya kuingizwa shambani au bandani.
Ø  Usiruhusu tabia ya kuchangia vifaa/vyombo kama vile makasha ya mayai, makreti ya kubebea kuku
kati ya shamba na shamba, n.k.
Ø  Wafanyakazi waanze kuwahudumia kuku wenye umri mdogo kabla ya wale wenye umri mkubwa.
Ø  Usiruhusu watoto kucheza na kuku.
Ø  Jaribu kuzuia idadi ya wageni wanaoingia shambani/bandani.
Ø  Weka utaratibu wa kuangamiza mizoga ya kuku.
Ø  Anzisha programu jumuishi ya kudhibiti wadudu/wanyama waharibifu.
Ø  Panga utaratibu mzuri wa kuwapa kuku huduma ya maji na kufanya usafi.
Ø  Panga utaratibu mzuri wa kuzoa taka na mizoga ya kuku.
Ø  Panga utaratibu mzuri wa kusafisha banda na kupulizia dawa.
Ø  Vifaa visafishwe na kuwekwa dawa ya kuua vijidudu kabla ya kuingizwa shambani.
Ø  Hakikisha magari yanapoingia shambani yanapita katika kidimbwi chenye dawa ya kuua vimelea
vya magonjwa.
Ø  Hakikisha mfanyakazi anabadilisha viatu/mabuti kabla ya kuingia katika kila banda
Ø  Weka taratibu nzuri za kuingia shambani, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha usafi wa viatu na mikono; au wageni na wafanyakazi kubadilisha nguo/viatu na kuvaa mabuti.





MAGONJWA MUHIMU YA KUKU/NDEGE WAFUGWAO

Ugonjwa ni nini? Ugonjwa ni mabadiliko kutoka katika afya ya kawaida ya mnyama/kuku. Hali hii hutokea pale
vimelea au vijidudu vinapoingia mwili wa mnyama, kwa kula vyakula vyenye sumu, au inapotokea kuna uhaba wa lishe au madini mwilini.



TOFAUTI ZA MUONEKANO KATI YA KUKU MWENYE AFYA NA KUKU MGONJWA

KUKU MWENYE AFYA NZURI
Ø  Macho na sura angavu
Ø  Hupenda kula na kunywa maji
Ø  Pua zilizo safi, upanga na undu mwekundu, manyoya
laini na yaliyopangika vizuri
Ø  Hupumua kwa utulivu
Ø  Sehemu ya kutolea haja huwa kavu
Ø  Kinyesi kikavu, cheupe na kisicho na rangi
Ø  Hutaga mayai kawaida

KUKU ASIYE NA AFYA NZURI
Ø  Huonekana mchovu na dhaifu
Ø  Hula na kunywa kidogo au zaidi ya kawaida
Ø  Hutoa kamasi puani, ute na matongotongo; manyoya
yaliyovurugika
Ø  Hupumua kwa shida na kwa sauti
Ø  Sehemu ya kutolea haja inakuwa na unyevunyevu na
kinyesi kuganda
Ø  Huharisha, kinyesi huwa na damu au minyoo
Ø  Hutaga mayai machache au husimama kutaga kabisa
Ø  Huwa na tabia ya kujitenga na wenzake katika kundi

No comments: